Wednesday 28 September 2016

TANGA NA UTALII

TANGA NA FURSA YA UTALII

Katika sekta ya utalii ni kama vile mji wa Tanga umesahaulika katika nchi ya Tanzania.Wengi wakielezea hutalii huelezea zaidi juu ya mbuga za wanyama na haswa hicho ndio kimefanywa kuwa ndio kivutio kikubwa cha utalii au uwepo wa mambo ya kale.Jambo hili ni upotofu wa hali ya juu.

Suala la utalii ni pana mno na utalii umegawika katika makundi anuai :

Utalii wa uwanda wa ardhi:Hii ni aina ya utalii ambapo watalii huajabia namna umbile la ardhi la sehemu fulani lilivyo mfano uwepo wa ardhi tambarare yenye nyasi ndogondogo au uwepo wa ardhi tambarare yenye changarawe ambayo imeenea eneo kubwa au uwepo wa milima mambonde makubwa yenye kustaajabisha ni vivutio vya utalii.

Tanga kwa hili tuna milima ya usambara ambayo INA jiografia kubwa na ya kuvutia Juhudi za kuitangaza LUSHOTO na AMANI katika kivutio hiki bado iko chini sana kiasi cha kuifanya TANGA kuonekana kama vile suala la utalii halina nafasi.

Utalii wa mito: Maporomoko ya maji kutoka katika maeneo ya juu ya mito ni kivutio kikubwa sana katika sekta ya utalii.Hili huonekana kama vile halina nafasi Tanga na kuonekana kama vile hakuna mito mikubwa na yenye maporomoko ya kustaajabisha kumbe Tanga tuna mto zigi ambao ndio tegemeo la maji ya kutumia katika jiji la Tanga mto huu hutokea juu kabisa kwenye milima ya usambara ambapo chemchem yake ndipo ilipoanzia.

Tuna mto Pangani ambao huu nao una mchango mkubwa katika kuzalisha umeme wa Taifa hili MTO huu mlango wake wa kuingilia bahari ya hindi hukutana na bahari na hakika maji ya mto huu hayachanganyiki na maji ya bahari.

Wangapi washalitangaza hili wangapi washalifanyia utafiti hili na kutangaza kivutio hiki cha utalii?

Maporomoko ya maji yaliyopo milima ya usambara nani ameyatangaza? Kituo cha kuzalisha umeme wa maji cha Pangani kilichopo Hale je ni nani amekitangaza? Kwa kawaida sekta ya utalii hukua katika eneo husika kulingana na namna wana jamii wanaoishi katika eneo husika wanavyoutangaza utalii wa kwao.Tusione maeneo yenye mbuga za wanyama kuwa ni kivutio kikubwa cha utalii ni kwasababu wenyeji wa maeneo hayo waliamua kuutangaza utalii huo na kuufanya kuwa ni sehemu ya ajira na kuwaingizia kipato.

Utalii wa bahari : Mungu katujaalia kuwa na fukwe kubwa sana lakini mpaka sasa utalii wa bahari bado haujajulikana na kutangazwa .Utalii wa bahari kuna visiwa vingi ndani ya bahari ya Hindi ukanda wa Tanga Tanga ambavyo vina historia kubwa na maajabu mengi sana mfano KISIWA MWEWE pwani ya MOA, KISIWA CHA MTANG'ATA PWANI YA TANGA,KISIWA CHA FUNGUNI PWANI YA TANGA  kama hatutaamua kuitangaza Tanga yetu na utalii hakuna atakayekuja kututangazia.

Utamaduni wa uvuvi na namna ya kuvua ni sehemu mojawapo ya utalii wa bahari ukanda wa Tanga una utamaduni wa asili katika kuvua ambapo ukiwaona wavuvi wakiitekeleza shughuli hii kwa tamaduni zao huwa ni yenye kuvutia .Nani atautangaza utalii wa Tanga kama sio mimi na wewe.? Migodi ya utengenezaji chumvi kilimo cha mwani hivi vyote ni vivutio vya utalii wa bahari.Fukwe ambazo tunazo ndani ya Mkoa huu wa Tanga zenye mandhar nzuri na za kuvutia lakini je zimetangazwaje? Tunashuhudia watu husafiri kuajabia ziwa Victoria lakini huwaoni kusafiri kuajabia maajabu ya bahari ya hindi katika upwa huu wa Tanga.Hii ni kwasababu hatujaamua kuifanya Tanga kuwa ni sehemu ya utalii.

Utalii ni tasnia inayotengenezwa,haitoshi tu kuwa na mazingira asilia bali ni kwa kiwango gani mazingira hayo yametengenezwa kuwa kivutio cha utalii?

Angalia utalii wa bahari unavyotengenezwa

Moja ,uwepo wa fukwe , ni lazima pia kuwepo na vifaa vya michezo na michezo inayoambatana na utalii wa fukwe kama viwanja vya michezo kandokando ya fukwe.Viwanja hivi huwa na mazingira yaleyale ya asili na hufuata kanuni zote za uhifadhi wa mazingira ya fukwe.

Pili, vifaa vya kuchezea majini kama ngalawa boya hizi ni ngalawa maalum ambazo hutumiwa kuchezea michezo ya ndani ya maji kwa kuyakata mawimbi.

Tatu, uwepo wa hotel nzuri za kisasa na zenye mandhari ya pwani zinazozingatia gharama kwa mtuvwa ndani na mgeni kutoka nchi nyingine.MFANO tunaona TICC MCHUKUUNI wamejaribu kufanya kitu cha namna hii na wageni huja wengi tu kuajabia mazingira ya bahari.

Bwawa la viumbe vya baharini, ni lazima kuwe na bwawa kubwa sana lililojengwa katika mandharu ya kuvutia ambapo linaweza kumsaidia mtu kuona kila aina ya samaki waliomo baharini na maisha yao kwa ujumla.Katika kulindeleza hili baadhi ya nchi wamejenga hotel ambazo ukiingia unaiona sehemu ya maji ya bahari na viumbe mbalimbali hili nalo ni sehemu mojawapo kubwa ya utalii wa bahari.Dubai katika utalii wa bahari wamefanikiwa mno.

Utalii wa mambo ya kale na utamaduni wa eneo husika.Tanga INA historia kubwa sana ndani ya nchi hii ya Tanzania lakini kwa kutoelezwa historian hiyo katika muktadha wa utalii ni kama vile imevizwa.Tuna makaburi ya wajerumani,Waingereza nakadhalika haya yakuelezwa katika muktadha wa utalii tayari tosha huwa ni kivutio cha utalii sisi ni matajiri w mambo ya kale lakini tumejidharau kwenye hili hakuna atakayetujua.Angalia mathalani Shule ya kwanza ya msingi Tanzania wakati huo Tanganyika ni Magila Shule ya kwanza ya sekondari ni Old Tanga nani kaziwekea sura ya utalii vitu hivi? Manispaa ya kwanza Tanganyika au Deutch Osta Afrika ilikuwa ni Tanga Nani kaiwekea sura ya utalii ?

Tuna kuta kubwa sana maeneo ya vijiji vingi vya pwani mathalani moa lakini je ni Nani kazielezea kuta au ngome hizi zilikuwa ni za nini?

Je waijua mashine ya kusaga unayotumia nguvu ya maji ambayo ilijengwa wakati wa mjerumani na mpaka leo hutumika kusaga nafaka eneo la mto zigi Amani? Je wajua kuwa kuna maua na miti pamoja na ndege ambao duniani kote hakuna wanapatikana Amani tu katika Mkoa wa Tanga?

Mwisho kabisa niseme kuwa hakuna mji unaokuwa kiutalii kama haujatangazwa na wenye mji husika na pia kama mazingira asilia yaliyopo hayajaekewa miundombinu ya kuufanya utalii ufanyike kwa kiwango cha hali ya juu.

Amarison Consultancy imedhamiria kuandaa vipindi vya TV kwa jili ya kuutangaza utalii wa Tanga na kila wilaya itatangazwa na kufamika vivutio vyake vya utalii tunaendelea kutengeneza vipindi vyetu wakati ukifika tutahitaji udhamini wa kuvirusha hewani kwenye TV  yoyote ile baada ya kutimiza vigezo na masharti.


              




2 comments:

  1. Je picha hii inayoambatana na mmaelezo haya ni moja kati ya mito (Zigi na Pangani) uliyoitaja?

    ReplyDelete